>Mwanzo >Masomo

Masomo

NGUVU YA NENO

Biblia inacho kile kiwezacho kumfanya Mkristo kuwa na nguvu ya kiroho na kiakili.  Mtunga Zaburi asema hivi,  “Kuyafafanusha maneno yako kwatia nuru, na kumfahamisha mjinga.”  Zaburi 119:130.  Biblia ni kitabu cha ajabu.  Ni historia inayotufunulia sisi mambo ya karne zile zilizopita.  Pasipo kuwa na  Biblia, sisi tungekuwa tumeachwa kufuata dhana mbalimbali na hadithi za uongo kwa habari ya matukio ya vizazi vile vilivyopita.  Ni unabii unaolifunua pazia la siku zijazo.  Ni Neno la Mungu, liufunualo mpango ule wa wokovu, ambalo linatuonyesha njia ile ambayo kwayo  sisi tunaweza kuikwepa mauti ile ya milele, na kujipatia wema wa milele na uzima wa milele.  Katika vitabu vyote vinavyoigharikisha [vinavyoijaza] dunia hii, haidhuru viwe vya thamani ilioje, Biblia ni Kitabu kipitacho vitabu vyote, inastahili kabisa kuwa somo letu na kupewa heshima.  Haitupatii sisi historia ya ulimwengu huu tu, bali maelezo ya ulimwengu ule ujao.  Ina mafundisho yahusuyo maajabu ya malimwengu mbalimbali;  inatufunulia katika ufahamu wetu tabia ya Mwasisi yule wa mbingu na nchi.  Ndani yake umo ufunuo wa Mungu kwa mwanadamu. Endelea kusoma

 

KUBADIRISHWA KWA NEEMA

Maombi ni njia iliyowekwa na Mbingu ya kupata ushindi katika pambano letu dhidi ya dhambi na katika kuikuza tabia yetu ya Kikristo.  Mivuto mitakatifu inayokuja kama jibu kwa maombi ya imani itafanikiwa kutenda kazi katika moyo wa mwombaji kwa kumpatia yale yote aombayo.  Kwa ajili ya kupewa msamaha wa dhambi, kwa ajili ya kupewa Roho Mtakatifu, kwa tabia ile inayofanana na ya Kristo, kwa ajili ya kupewa hekima na nguvu ili kufanya kazi yake, kwa kipawa cho chote alichotuahidi, tunaweza kuomba;  na ahadi yake ni hii,  “Mtapokea.”

     Ilikuwa ni katika mlima ule, akiwa pamoja na Mungu, Musa alipokiona kiolezo cha jengo lile la ajabu ambalo lilikusudiwa kuwa maskani ya kukaa utukufu wa Mungu.  Ni katika mlima tukiwa pamoja na Mungu  -  katika mahali petu pa faragha pa maombi  -    tunapopaswa kuutafakari mfano ule ulio bora kwa wanadamu.  Endelea kusoma

 

 

YANIPASA NIFANYE NINI ILI NIPATE KUOKOKA?

     Wakati ambapo wokovu wetu hutegemea kabisa juu ya Yesu, bado sisi tunayo kazi ya kufanya ili tupate kuokoka.  Mtume anasema,  “Utimizeni wokovu wenu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.  Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema” (Wafilipi 2:12,13).  Kazi tunayotakiwa kufanya si kazi ya kujitegemea wenyewe mbali na kazi ile anayotaka kufanya Mungu [ndani yetu], bali ni kazi ya kushirikiana na Mungu.  Uweza na Neema ya Mungu hutumiwa na Mtendakazi huyo wa Mbinguni ndani ya moyo;  lakini hapa ndipo wengine hupotea, wakidai kwamba mwanadamu anayo kazi ya kufanya ambayo ni ya kujitegemea mwenyewe kabisa bila kushirikiana na kazi yo yote anayotenda Mungu [ndani yake].  Kundi lingine huvuka mpaka na kwenda upande mwingine, na kusema kwamba mwanadamu hawajibiki kabisa, ati kwa sababu Mungu anafanya kazi yote  -  kutaka na kutenda.  Lakini sababu ya kweli tunayotakiwa kuifuata ni ile isemayo kwamba nia [mapenzi] ya mwanadamu inapaswa kuitii nia [mapenzi] ya Mungu.  Nia ya mwanadamu haipaswi kulazimishwa ili ipate kushirikiana na  wajumbe wale aliowaweka Mungu, bali inapaswa kunyenyekea kwa hiari.  Mwanadamu hana uwezo wo wote ndani yake wa kumwezesha kuutimiza wokovu wake mwenyewe.  Endelea kusoma

 

 

KUKABIRIANA NA KUMBUKUMBU ZA MAISHA YETU

 

Kazi ya kila mtu inachunguzwa mbele za Mungu na inaandikwa kama ni ya UAMINIFU ama ya KUKOSA UAMINIFU. Mbele yake kila jina katika vitabu vya mbinguni huandikwa kwa usahihi kabisa kila neno baya, kila tendo la uchoyo [ubinafsi], kila kazi isiyotimizwa, na kila dhambi ya siri, na kila unafiki uliofanywa kwa werevu. Maonyo yaliyotumwa kutoka mbinguni na makaripio YALIYOPUUZWA, wakati uliopotezwa bure [kucheza karata, bao, n.k.], nafasi ambazo hazikutumiwa vizuri, mvuto uliotolewa kwa WEMA au kwa UBAYA, pamoja na matokeo yake yafikayo mbali, vyote hivi vinawekwa katika kumbukumbu zenye tarehe na malaika yule anayetunza kumbukumbu hizo. Endelea kusoma

 

KATIKA ROHO NA NGUVU YA ELIA

 

Kupitia katika karne ndefu zilizopita tangu wakati ule wa Eliya, kumbukumbu ya kazi yake ya maisha imewatia nguvu na ujasiri wale walioitwa kuitetea haki katikati ya uasi.  Na kwetu sisi, “tuliofikiliwa na miisho ya zamani” hizi (1 Wakorintho 10:11), ina maana ya pekee.  Historia inajirudia yenyewe.  Ulimwengu leo unao akina Ahabu wake na akina Yezebeli wake.  Kizazi cha sasa ni kimoja ambacho kinaabudu sanamu, ni sawa kabisa na kile alichoishi Eliya.  Hakuna madhabahu inayoweza kuonekana kwa macho;  huenda pasiwepo na sanamu yo yote ambayo jicho linaweza kuitazama, lakini bado maelfu wanaifuata miungu ya ulimwengu huu  -  yaani, wanafuata utajiri, sifa, anasa, na hadithi za uongo zinazopendeza ambazo zinamruhusu mwanadamu kufuata mielekeo ya moyo wake ambao haujazaliwa mara ya pili.  Watu wengi sana wana dhana potofu kuhusu Mungu na sifa zake, nao, kusema kweli, wanamtumikia mungu wa uongo kama vile walivyofanya wale waliomwabudu Baali.  Wengi, hata miongoni mwa wale wanaojiita Wakristo, wamejifungamanisha wenyewe na mivuto ile inayompinga Mungu na kweli yake bila [kuonyesha] badiliko lo lote.  Hivyo ndivyo wanavyoongozwa kumpa Mungu kisogo na kumtukuza mwanadamu. Endelea kusoma